SOMO LA KWANZA
1 Samueli 16:1—13
Somo katika kitabu cha kwanza cha Samueli
Siku zile: Bwana alimwambia Samueli: "Utamlilia Sauli hata lini, ikiwa mimi nimesema asitawale Israeli tena? Uijaze pembe yako mafuta, uende. Nami ninakutuma kwa Yese, mtu wa Bethlehemu, maana nimejichagulia mfalme kati ya wanawe." Samueli akasema, "Nitawezaje kwenda? Maana Sauli akipata habari ataniua!" Bwana akamjibu: "Chukua ndama pamoja nawe na useme, 'Nimekuja kumtolea Bwana sadaka.' Utamwalika Yese aje kushiriki kwenye sadaka, nami nitakuonyesha utakavyopaswa kutenda; na utampaka mafuta kwa jina langu yule nitakayemtaja kwako. Basi Samueli akafanya kama alivyoamriwa na Bwana. Alipofika Bethlehemu wazee wa mji wakaenda kumlaki, huku wakitetemeka na kusema, "Ujio wako hapa ni wa amani, ewe mwonaji?" Samueli akajibu, "Ndiyo, nimekuja kwa amani, kumtolea Bwana sadaka. Jitakaseni, na njoni pamoja nami kwenye sadaka." Akawatakasa Yese na wanawe, na kuwaalika kwenye sadaka. Walipofika, alimtazama Eliabu, akasema, "Hakika mpakwa wa Bwana yupo hapa mbele yake." Lakini Bwana akamwambia Samueli: Usiutazame uso wake, wala urefu wa kimo chake, kwa maana nimemkataa. Kwa maana Mungu haangalii kama binadamu anayoangalia: maana mwanadamu anatazama sura ya nje, lakini Bwana hutazama moyo. Yese akamwita Abinadabu na kumpitisha mbele ya Samueli, naye akasema, "Bwana hakumchagua huyu." Tena Yese akampitisha Shama, na Samueli akasema, "Wala Bwana hakumchagua huyu." Kisha Yese akawapitisha wanawe saba mbele ya Samueli. Samueli akamwambia Yese, "Bwana hakuchagua hata mmoja kati yao." Akamwambia Yese, "Hawa ndio vijana wako wote?" Naye akajibu, "Mdogo wao amebaki, anawachunga kondoo." Samueli akamwambia Yese, "Tuma mtu amlete, maana hatutaketi mezani mpaka atakapokuja huku." Basi akamtuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo la kupendeza. Ndipo Bwana akasema: Simama, umpake mafuta maana huyu ndiye. Samueli akaitwaa pembe yenye mafuta, akampaka mafuta kati ya ndugu zake, na tangu siku ile Roho wa Bwana akamjia Daudi kwa nguvu. Kisha Samueli akaondoka, akaenda zake Rama.
Neno la Bwana.
ZABURI YA KUITIKIZANA
ZABURI 89:20, 21—22, 27—28 (K. 21a)
K. Nimemchagua Daudi, mtumishi wangu.
Awali uliwaambia waaminifu wako katika maono, ukasema:
"Nimempa aliye hodari msaada,
nimemkuza kijana kutoka miongoni mwa watu. K.
Nimempata Daudi, mtumishi wangu;
nimempaka mafuta yangu matakatifu.
Mkono wangu utakuwa tegemeo lake;
mkono wangu utamtia nguvu. K.
Yeye ataniita, 'Wewe ni Baba yangu,
Mungu wangu na mwamba wa wokovu wangu.'
Nami nitamweka awe mzaliwa wangu wa kwanza,
aliye juu sana kuliko wafalme wa dunia." K.
SHANGILIO LA INJILI
Waefeso 1:17—18
K. Aleluya. W. Aleluya.
K. Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, ayatie nuru macho ya mioyo yetu ili tupate kujua tumaini tuliloitiwa.
W. Aleluya.
INJILI
Marko 2:23—28
Somo la Injili takatifu ilivyoandikwa na Marko.
Yesu alipita mashambani siku ya Sabato, wafuasi wake walipokuwa wakipita, wakaanza kupura masuke ya nafaka. Hapo Mafarisayo wakamwambia, "Tazama, kwa nini wanafanya iliyo haramu siku ya Sabato?" Naye akawaambia, "Je, hamkusoma alichofanya Daudi alipopatwa na shida ya kuwa na njaa, yeye na wenziwe? Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu wakati Abiathari alipokuwa kuhani mkuu, akaila mikate ya Wonyesho, ambayo ni haki ya makuhani tu kuila, tena akawapa na wale waliokuwa pamoja naye?" Akawaambia, "Sabato ilikuja kwa ajili ya watu, si watu kwa ajili ya Sabato. Basi, Mwana wa Mtu ni Bwana wa Sabato pia."
Injili ya Bwana.