SOMO 1
Isaya 2:1—5
Haya ndiyo aliyoyaona Isaya, mwana wa Amosi, kuhusu Yuda na Yerusalemu. Itatukia siku za mwisho ya kuwa mlima wa hekalu la BWANA utawekwa imara juu ya milima, na kuinuliwa juu kupita vilima. Mataifa yote watauendea kwa wingi. Na makabila mengi watafika huko, wakisema, "Haya, tuupande mlima wa BWANA, tuiendee nyumba ya Mungu wa Yakobo, ili atufundishe njia zake, nasi tufuate mapito yake." Maana toka Sioni sheria itatokea, na neno la BWANA kutoka Yerusalemu. Naye atafanya hukumu kati ya mataifa, atawaamua makabila mengi. Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao kuwa mapanga; taifa halitainua upanga juu ya taifa jingine, wala hawatajifunza ufundi wa vita tena. Enyi watu wa nyumba ya Yakobo, njooni, tutembee katika mwanga wa BWANA!
Neno la Bwana.
ZABURI YA KUITIKIZANA
ZABURI 122:1—2, 3—4a, 8—9 (K. tazama 1)
K. Kwa furaha tutaingia nyumbani mwa Bwana.
Nalifurahi waliponiambia,
"Twende nyumbani kwa Bwana."
Sasa miguu yetu imesimama
ndani ya malango yako, ee Yerusalemu. K.
Yerusalemu uliojengwa
kama mji ulioshikamana.
Ndiko wanakopanda makabila,
makabila ya Bwana. K.
Kwa ajili ya ndugu zangu na rafiki zangu,
nitasema, "Amani kwako."
Kwa ajili ya nyumba Bwana, Mungu wetu
naomba "Neema ziwe kwenu." K.
SHANGILIO LA INJILI
ZABURI 80:4
K. Aleluya. W. Aleluya.
K. Ee Bwana Mungu wetu, uturudishe tena, utuangazie uso wako, nasi tutaokoka.
W. Aleluya.
INJILI
Mathayo 8:5—11
Wakati ule: Yesu alipokuwa akiingia Kapernaumu, akida mmoja alimjia, akamwomba akisema, "Bwana, mtumishi wangu amelala nyumbani, mgonjwa wa kupooza, anaumwa sana." Yesu akamwambia, "Nitakuja kumponya." Akida akamjibu akisema, "Bwana, sistahili uingie chini ya dari yangu; lakini useme neno tu na mtumishi wangu atapona. Hata mimi niliye mtu chini ya amri nina askari chini yangu. Nikimwambia mmojawapo, 'Nenda,' huenda; na mwingine, 'Njoo,' huja; na nikimwambia mtumishi wangu, 'Fanya hivi,' hufanya." Yesu aliposikia hayo, alishangaa, akawaambia wale waliomfuata, "Amin, nawaambieni, sijapata kuniona imani kubwa kama hiyo kwa yeyote katika Israeli. Lakini nawaambieni, wengi watakuja kutoka mashariki na magharibi na kukaa mezani na Abrahamu na Isaka na Yakobo katika ufalme wa mbinguni."
Injili ya Bwana.